MAFIA
Wakala ya Barabara za
Vijijiji na Mijini (TARURA) Wilaya ya Mafia kwa mwaka wa fedha 2023/24
imefungua jumla ya barabara mpya 10 zenye urefu wa kilomita 34.6 ili kuwezesha
wananchi kuyafikia maeneo yaliyokuwa hayafikiki.
Hayo yamebainishwa na
Meneja wa TARURA Wilaya ya Mafia Mhandisi Maneno Makorongo wakati wa ukaguzi wa
miradi inayotekelezwa wilayani humo.
"TARURA Wilaya ya
Mafia hadi sasa tumefungua barabara mpya 10 kwa mwaka huu wa fedha na hii ni
sehemu ya utekelezaji wa mpango mkakati
wetu wa kuhakikisha tunafungua barabara kufika kusiko fikika", amesema
Mhandisi Maneno.
Naye Diwani wa Kata ya
Baleni, Mhe. Darweshi Abedi amesema kuwa barabara hiyo ina mchango mkubwa kwa
wananchi kwani itasaidia katika shughuli za kijamii na kiuchumi ikiwa ni pamoja
na kuwezesha wananchi kusafirisha mazao kwa urahisi kuelekea sokoni.
"Barabara hii ya
Zawiani-Mlola ni muhimu kwa uchumi wetu maana ukiacha kusafirisha mazao bado
kuna shughuli za kijamii zinazotegemea uwepo wa usafiri wa uhakika kwa kipindi
chote cha mwaka", amesema Mhe. Darweshi
Kwa upande wake Bi.
Mwanaisha Omary ambaye ni mkazi wa Kijiji cha Kungwi ameeleza kuwa suala la
kuifungua barabara ya Zawiani-Mlola yenye urefu wa kilomita 2.6 imeleta fursa
kwa wananchi kijamii na kiuchumi na kwamba eneo hilo halikuwahi kuwa na
barabara.
"Mwanzoni
hatukuamini juu ya ufunguzi wa barabara hii lakini sasa shughuli za kiuchumi
zinaendelea vizuri na hata zile za kijamii kwani ni rahisi kuzifikia huduma za
afya na elimu tofauti na awali, tunaipongeza serikali kwa kuuona umuhimu wa
barabara hii", amesema Bi. Mwanaisha
Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA ) katika Wilaya ya Mafia mkoani Pwani hadi sasa inasimamia mtandao wa Barabara zenye urefu wa kilomita 208 lengo likiwa ni kuendelea na ujenzi na matengenezo ya barabara hizo ili kuwezesha wananchi kufika kusiko fikika.
0 Comments