TANZANIA NA UGANDA ZATIA SAINI MKATABA MAHSUSI



Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya

Uganda zimetia saini mkataba mahsusi utakaowezesha kuanza kwa kazi ya

upembuzi yakinifu wa Mradi wa Ujenzi wa Bomba la Kusafirisha Gesi

kutoka Tanzania kwenda Uganda.

Mkataba huo umesainiwa leo jijini Dodoma na Naibu Waziri Mkuu na

Waziri wa Nishati wa Tanzania, Mhe. Dkt. Doto Biteko pamoja na Mhe.

Ruth Nankabirwa, Waziri wa Nishati na Maendeleo ya Madini wa Jamhuri

ya Uganda.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt.Doto Biteko amesema kuwa,

kusainiwa kwa Mkataba huo kumetokana na  Makubaliano ya Awali

(Memorandum of Understanding - MoU) kati ya nchi hizi mbili

yaliyosainiwa mwezi Agosti, mwaka 2018  kwa ajili ya ujenzi wa Bomba

la kusafirisha Gesi Asilia kutoka Tanzania kwenda Uganda kutokana na

Tanzania kugundua kiasi kikubwa cha gesi katika kina kirefu cha bahari

na nchi kavu.

“ Nchi hizi mbili zimekubaliana kufanya kazi ya upembuzi yakinifu kwa

pamoja kuwezesha tathmini ya mradi na kutoa muongozo wa uwezekano wa

mradi ikiwemo muundo wa mradi, mahitaji ya gesi, ukubwa wa bomba na

taarifa  nyingine muhimu zinazohusu mradi huo kwa ajili ya kufanya

maamuzi.” Amesema Dkt. Doto Biteko

Dkt. Biteko amesema kuwa, Nishati ni ufunguo wa maendeleo kwa nchi

yoyote ile duniani na umoja ni nguvu hivyo ametoa wito kwa nchi hizi

mbili kutumia fursa ya kutekeleza mradi huu ambao utaunganisha nchi

hizi mbili katika nyanja ya kiuchumi na kijamii.

Amesema kuwa, licha ya Tanzania kugundua kiasi kikubwa cha gesi asilia

takiriban futi za ujazo trilioni 57.54, mahitaji ya rasilimali hii

yanakua kwa kasi ndani na nje ya nchi na hii inapelekea Serikali

kuweka nguvu zaidi katika utafutaji kwa lengo la kuongeza upatikanaji

wa nishati hiyo katika maeneo mbalimbali ikiwemo Eyasi Wembere, Mnazi

Bay Kaskazini, Songosongo Magharibi, Ziwa Tanganyika na katika kina

kirefu cha maji baharini.

Ameongeza kuwa, Tanzania inaendelea kutafuta wabia wa kimkakati

watakaoweza kushirikiana na Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania

(TPDC) ili kutafiti na kuendeleza vyanzo vya upatikanaji wa mafuta na

gesi.

Pamoja na kupongeza timu zilizofanya kazi hadi kupelekea kusainiwa kwa

mkataba huo, ameagiza kuwa kazi zilizopangwa kufanyika baada ya

kusainiwa kwa mkataba huo zifanyike kwa wakati ikiwemo upatikanaji wa

Mshauri Mwelekezi wa kufanya kazi hii na kila upande unapaswa kuona

kuwa mradi huo ni wa kipaumbele.

Kwa upande wake, Waziri wa Nishati na Maendeleo ya Madini kutoka

nchini Uganda Mhe. Ruth Nankabirwa amesema kuwa, Uganda inatambua

umuhimu wa mradi huu na kuongeza kuwa kumekuwepo na mahitaji makubwa

ya matumizi ya gesi hivyo wana kila sababu ya kuhakikisha kunakuwepo

na uharakishwaji wa mradi huo.

Ameitaka Kamati ya pamoja ya utekelezaji wa Mradi huo kuhakikisha

wanaharakisha mchakato wa manunuzi ya Mshauri Mwelekezi wa mradi ili

kuharakisha upembuzi yakinifu tayari kwa utekelezaji.

Aidha, amesema Tanzania na Uganda zimekuwa zikishirikiana katika

miradi mbalimbali kwenye sekta ya Nishati ikiwemo Mradi wa uzalishaji

wa umeme wa maji Megawati 14 wa Kikagati, mradi wa kusafirisha umeme

kutoka Masaka Mutukula hadi Mwanza na mradi wa Bomba la Mafuta ambalo

waliona lipite Tanzania.

Hafla hiyo, ilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo Makatibu

Wakuu wa Wizara za Nishati kutoka nchi zote mbili, makamu Mwenyekiti

wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Balozi wa Uganda

nchini Tanzania,  Wakuu wa taasisi zilizo chini ya Wizara hizo ikiwemo

TPDC, EWURA, PURA na UNOC na wawakilishi wa Wizara ya Fedha, Wizara ya

Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Ofisi ya

Mwanasheria Mkuu wa Serikali.


Post a Comment

0 Comments