Kero ya Mafuta na Umeme yatinga vikao vya juu CCM


 

*Wajumbe wa Halmashauri Kuu wataka maelezo ya kina utatuzi wake, Mawaziri wajieleza, ufuatiliaji kufanyika kwa karibu zaidi

 

Na. Mwandishi wetu

 

HALMASHARI Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Chama Cha Mapinduzi (CCM), imeelekeza kupatiwa ufumbuzi wa haraka wa kero ya kukatika kwa umeme, upungufu wa mafuta ambao huwa unajitokeza ingawa si mara kwa mara na changamoto ya bei ya mazao ya kilimo.

 

Pia, katika kikao cha NEC kilichofanyika Novemba 29, mwaka huu, jijini Dar es Salaam, wajumbe walijadili kuhusiana na huduma za afya, hususani kwa wazee, wajawaziti na watoto, pamoja na    mpango wa bima ya afya kwa wote.

 

Hayo yalielezwa Novemba 30, 2023 na Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Abdulrahman Kinana, alipozungumza na wananchi wa Jimbo la Rufiji, mkoani Pwani, katika mkutano ulioandaliwa na mbunge wa jimbo hilo, ambaye ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mohamed Mchengerwa, kueleza utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2020-2025.

 

"Chini ya Mwenyekiti Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kile kikao (NEC) kilifanyika siku nzima, mambo yote tuliyojadili ni yale yaliyohusu wananchi, tulijadili kuhusu kukatikatika kwa umeme, tatizo la mara moja moja la upungufu wa mafuta, tatizo la bei ya mazao; korosho, pamba, tumbaku, kahawa, alizeti na mengine yote," alisema Kinana.

 

Alisema, Rais Dkt. Samia alimtaka Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, kutoa majibu ya hoja zilizotoka kwa wajumbe wa NEC ambapo alifanya hivyo, akisaidiwa na mawaziri wakiwemo Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigilu Nchemba, Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe, Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu na Waziri wa Maji, Jumaa Aweso.

 

Ndugu Kinana, alisema kwamba wajumbe wa kikao hicho walizungumzia utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa upande wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar.

 

Alisema, Mwenyekiti wa CCM Dkt. Samia, alimtaka Makamu wa Pili wa Rais, Hemed Suleiman Abdulla  kutoa taarifa kuhusu utekelezaji wa ilani.

 

Kinana alisema, Mwenyekiti alisisitiza changamoto zilizozungumzwa na wajumbe wa NEC kuhusiana na sekta mbalimbali zipatiwe ufumbuzi mapema iwezekanavyo kama alivyowahi kuagiza siku za nyuma.

 

"Mambo haya utekelezaji wake utafuatiliwa kwa karibu na Mwenyekiti mwenyewe," alisisisitiza Makamu Mwenyekiti Kinana.

Post a Comment

0 Comments