Waathirika wa mafuriko Hanang kusaidiwa na wadau wa COP28

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amewahakikishia wakazi wa mji mdogo wa Katesh walioathirika na mafuriko makubwa kuwa serikali itarejesha huduma zote za msingi za kijamii.

Rais Samia amesisitiza kuwa serikali itaendelea kufanya tathmini ya uharibifu wa mali huku akiiagiza Wizara ya Nishati kuangalia uwezekano wa upatikanaji wa umeme wa dharura baada ya miundombinu kuharibika na maafa haya ili shughuli za uopoaji zifanyike usiku na mchana.

Rais Samia ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na wananchi na waathirika mara baada ya kutembelea maeneo yaliyoathirika na mafuriko hayo na kushuhudia hali halisi ya uharibifu wa maafa.

Mkuu wa mkoa wa Manyara Queen Sendiga akitoa maelezo kwa Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kuhusu mafuriko na maporomoko ya tope kutoka mlima Hanang yaliyogharimu maisha ya makumi ya wakazi wa wilaya ya Hanang mkoani Manyara.

Aidha Rais Samia ameongeza kuwa mbali na michango mbalimbali iliyotolewa ndani ya nchi lakini pia kumetolewa takriban Shilingi bilioni 2.5 kutoka kwa wahisani walioshiriki kwenye mkutano wa COP 28, Dubai.

Miongoni mwa maeneo aliyotembelea Rais Samia ni Hospitali ya Tumaini wilayani humo kwa ajili ya kuwajulia hali na kuwafariji majeruhi na pia shule ya Sekondari ya Katesh ambapo ndipo makazi ya muda yalipowekwa ili kuwastiri waathirika hao.

Vile vile, Rais Samia ametaka tahadhari zote za msingi zichukuliwe ili  kusitokee janga jingine la mlipuko wa magonjwa hivyo kuheshimu kanuni za usafi kwani amesema majanga wakati mwengine huzua maradhi kama kipindupindu.

Tazama Rais akiwafariji waathirika wa mafuriko Hanang na kuahidi kutoa misaada zaidi

Hivyo Rais Samia ameielekeza Wizara ya Maji kuhakikisha huduma za maji safi na salama zinaendelea kupatikana muda wote huu hususan maeneo yaliowekwa makambi ya kustiri waathirika wa janga hilo.

Mafuriko mazito yaliotokea yamesababisha vifo vya Watanzania 76 hadi sasa, huku kaya 1,150 zikiwa  zimeathirika na watu 5,600. Pia kumekuwa na majeruhi zaidi ya 117 pamoja na uharibifu wa miundombinu ya barabara, maji na umeme.

Post a Comment

0 Comments