Askofu ataka serikali idhibiti "Kamchape"

 


Askofu wa kanisa la Anglikana jimbo la magharibi Kasulu (Diocese of western Tanganyika) mhashamu Emanuel Bwata ametoa wito kwa serikali kuchukua hatua za haraka kudhibiti vitendo vya kishirikina na uporaji vinavyofanywa na watu wanaojiita kuwa kundi la kamchape

Wito huo ameutoa leo wakati wa ibada maalumu ya kumbukizi za kuanzishwa kwa jimbo hilo iliyofanyika katika kanisa kuu la mtakatifu Andrea mjini Kasulu ambapo Mkuu wa Wilaya Kanali Isack Mwakisu, Profesa Joyce Ndalichako mbunge wa jimbo la Kasulu mjini pamoja na Josepbine Genzabuke mbunge wa viti maalumu walikuwa sehemu ya waumini katika kanisa hilo.

Askofu Bwata amebainisha kuwa kikundi hicho kinaendesha wizi, uporaji na unyang’anyi wa mali na kuchochea chuki miongoni mwa wanajamii kwa kisingizio cha kutoa uchawi majumbani huku wakijinasibu kuwa na mamlaka juu ya mtu yeyote.

Ukimya wa serikali dhidi ya hao wanaojiita kamchape ndio unaowapa nguvu za kuendelea kutenda uhalifu huo unaochochea chuki na udhalilishaji kwa jamii, mbaya zaidi wanataja kuwa na vibali kutoka juu, ikiwemo kuhusisha jina la Rais” Anaeleza Askofu Bwata.

Askofu Emanuel Charles Bwata wa kanisa kuu la uaskofu wa Diocese of Western Tanganyika akihubiri katika kanisa hilo ambalo kwa sasa linakarabatiwa

Askofu Bwata amebainisha watu hao ambao hadi sasa hawajakamatwa wamekuwa wakitumia jina la Rais Samia Suluhu Hassan kuendesha uhalifu kwa kisingizio cha kutoa uchawi kwa wananchi katika mkoa wote wa Kigoma na kwamba wamefikia hatua ya kutishia kuvamia makanisa.

Tunajua wapo wachawi na wapo wagaga wa jadi ambao hutenda mambo yao kulingana na Imani yao, kazi yetu sisi ni kuwahubiria neno la Mungu ili wamfuate Yesu, lakini hao kamchape siyo waganga maana vitendo vyao ni vya uporaji wa mali za wananchi” Anasisitiza Askofu Bwata.

Katika hatua nyingine Askofu Bwata ametoa wito wa kufanyika kwa chaguzi za viongozi wa serikali kwa kizingatia maadili na kuepuka vitendo vya rushwa miongoni mwa wagombe.

Amehimiza waumini wa kanisa hilo kujitokea kugombea nafasi za uongozi katika serikali za mitaa na katika uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais utakaofanyika 2025, huku akionya wagombea wanaohonga wapigakura.

Ni aibu na dharau kubwa kwa wananchi kumchagua mtu ambaye anahonga chumvi na mavazi hususani fulana, kofia na vitenge badala ya kujenga hoja na kutangaza sera juu ya namna atakavyowatumikia wapiga kura, mimi kama askofu katika huduma zangu baada ya tume ya uchaguzi kutangaza kuanza kwa mchakato wa uchaguzi, nitawafundisha na kuwaelekeza waumini njia sahihi za kupata viongozi bora” Amesisitiza Askofu Bwata.

FUATILIA MJADALA KWENYE TWITTER YA BUHA FM RADIO HAPA

Aidha askofu Bwata ametumia muda huu kuitaka serikali kuwaacha huru wananchi kugombea na kuchagua viongozi wanaowataka bila kujali wanatoka vyama gani vya siasa akitaja kuwa hiyo ndiyo demokrasia sahihi.

Amehitimisha hotuba yake kwa kutoa wito kwa serikali kuweka wazi mchakato wa maoni ya sheria za uchaguzi, mchato wa Katiba mpya na sheria za vyama wa siasa akidai kuwa sheria pamoja na katika ni mali ya wananchi hivyo uwepo uhuru kwa kila mwananchi kushiriki badala ya wanasiasa kugeuza michakato na mipango ya serikali kama mali yao.

Mkuu wa Wilaya ya kasulu Kanali Isack Mwakisu akifafanua kuhusu msimamo wa serikali kwenye masuala mbalimbali ya ulinzi nz usalama katika wilaya yake

Akijibu baadhi ya hoja za Askofu Bwata, Mkuu wa wilaya ya Kasulu Kanali Isack Mwakisu amewaeleza wananchi wa Kasulu kuwa serikali hairuhusu vitendo vya Kamchape na hatua mbalimbali za kisheria zimekuwa zikichukuliwa dhidi ya wafuasi na mashabiki wa kikundi hicho

Serikali haiungi mkono uhalifu na hao kamchape ni wahalifu, Rais Samia hajawatuma na hawezi kufanya upuuzi huo, hao ni wahalifu na wanatoa kauli hizo ili kuichafua heshima ya Rais na heshima na amani ya nchi yetu, hivyo wapuuzeni” amesisitiza Mkuu wa wilaya ya Kasulu Kanali Isack Mwakisu.

Kanali Mwakisu ametoa onyo kwa wanaojihusisha au kushabikia Kamchape kuacha mara moja, huku akitoa wito kwa wananchi kutoa taarifa kwa mamlaka za serikali ikiwemo vyombo vya dola endapo watawabaini wanaojihusisha na vitendo hivyo.

Naye Mbunge wa jimbo la Kasulu mjini Profesa Joyce Ndalichako aliyekuwa mgeni rasmi katika Ibada hiyo amelipongeza kanisa la Anglikana kwa namna wanavyotoa ushirikianoo kwa serikali katika kutekeleza afua mbalimbali za maendeleo Pamoja na kuhubiri amani

Profesa Ndalichako amebainisha kuwa kanisa lina mchango mkubwa katika kuisaidia serikali kutekeleza wajibu wake wa kuhudumia wananchi na kuimarisha usalama katika jamii nan chi kwa ujumla.

Profesha Joyce Ndalichako akihutubia waumini wa kanisa kuu la Anglikana Kasulu mjini na kuhimiza jamii kulinda amani na kufanya kazi kwa bidii

Akieleza kuhusu masala ya ajira, Ndalichako amewajulisha watanzania kuwa serikali inaendelea na mipango yake ya uwezeshaji jamii kiuchumi kupitia Nyanja mbalimbali ikiwemo mfuko wa asilimia 10 za mapato ya ndani ya halmashauri ambao hutoa mikopo kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu ambao wameanzia vikundo na miradi ya maendeleo.

“Serikali inaendelea na maboresho mbalimbali ya mifuko ya uwezeshaji jamii kiuchumi, hivyo ni wajibu wa kila mwananchi kubuni mradi na kufanya kazi kwa bidi ili kujiletea maendeleo na kuepuka utegemezi” amebainisha Prof. Ndalichako Mbunge

Amesisitiza kuwa miradi ya kimkakati inayoendelea kujengwa wilayani Kasulu na katika mji wa Kasulu ukiwemo umeme, Barabara na maji, ni sehemu tu ya mipango ya serikali kuhakikisha jamii inapata huduma za kijamii kwa ubora zaidi.

“Nikitazama nilivyolipokea jimboa la kasulu na hali ilivyo sasa naona fahali sana maana mambo yamebadilika na kuna miradi mingi imefanyika hususani sekta ya afya, elimu, miundombinu na maji, sina budi kumpongeza mheshimiwa Rais kwa utoaji wa fedha nyingi za maendeleo kwa ajili ya jimbo letu na mkoa wetu kwa ujumla. Anabainisha Mh. Ndalichako

Profesa Ndalichako, kanali Mwakisu na Josephine Genzabuke wakisikiliza hotuba ya mhashamu askofu Emanuel Bwata

Kuhusu Imani za kishirikina, profesa Ndalichako ametoa wito kwa viongozi wa kanisa kuendelea kukemea na kutoa elimu ili watu wanaoamini ushirikiana wageuze mienendo yao.

Aidha Profesa Ndalichako amewataka wazazi kuhakikisha Watoto wote wanaotakiwa kujiunga na shule za awali, msingi na sekondari kidato cha kwanza kuhakikisha wanawapeleka kuanza masomo.

Picha ya pamoja ya Askofu Emanuel Bwata, Mbunge wa Kasulu mjini prof. Joyce Ndalichako, Mbunge viti Maalum Josephine Genzabuke, Mkuu wa wilaya Kasulu Kanali Isack Mwakisu pamoja na ma- Kanoni walei wapya ambao wametawazwa kuwa washauri wa viongozi wa kanisa hilo katika maeneo yao

Kanisa la Anglikana jimbo la magharibi lenye makao makuu mjini Kasulu, linaongoza waumini wa kanisa hiyo katika mikoa ya Rukwa, Katavi, Tabora na Kigoma na linatimiza nusu karne tangu manisa kuu kujengwa.

 

 

 

Post a Comment

0 Comments