Mwanza yazizima ziara ya Rais Samia

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan ameitaka Wizara ya Mifugo na Uvuvi kushirikiana na Sekretarieti za Mikoa na Halmashauri kudhibiti na kutokomeza vitendo vya uvuvi haramu.

 

Rais Samia ameyasema hayo leo wakati akihutubia wananchi katika uwanja wa Nyamagana mara baada ya kuzindua na kukabidhi boti za uvuvi na vizimba vya kufugia samaki kwa wavuvi wa kanda ya ziwa.

 

Aidha, Rais Samia ameitaka Wizara hiyo kuwachukulia hatua kali za kisheria  wavuvi wanaokiuka taratibu za uvuvi salama.


Rais Samia pia amesema serikali inafanya jitihada kuinua sekta ya uvuvi nchini kwa kuimarisha utendaji wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi ili iendane na dhamira ya mageuzi yaliyokusudiwa.

 

Vile vile, Rais Samia amesema kundi la vijana na wanawake linaongoza kushiriki kwenye ajira zisizo rasmi hivyo serikali inarasimisha shughuli zao kwa kuwawezesha kupata zana na nyenzo za kisasa ili kujikimu kiuchumi.

 

Rais Samia amesema serikali imejipanga kukuza sekta ya uvuvi kupitia miradi mbalimbali  ikiwemo ununuzi wa meli za kisasa za uvuvi katika bahari kuu, ujenzi wa bandari za uvuvi katika maeneo ya Kilwa Masoko mkoani Lindi na Bagamoyo ili kuongeza pato la taifa.

 

Boti 160 za uvuvi wa kisasa zimezinduliwa kwa wanufaika 989 pamoja na vizimba 222 vinavyotarajiwa kugaiwa kwa wanufaika 1,213 katika mikoa ya Mwanza, Mara, Kagera, Simiyu na Geita.  

 

Post a Comment

0 Comments