Fundi vyuma na umeme aunda Pikipiki Kakonko, Kigoma

Je umewahi kufikiri kuwa kazi za ubunifu zinaweza kufanyika pia kijijini na kwa watu wenye elimu ya wastani? Kama kama jibu lako ni Hapana ukweli wa mambo tunao leo katika kurunzi ya DW ambayo imezuru mkoani Kigoma magharibu mwa Tanzania

Kijana mmoja mwenye fani ya ufundi anayefaham,ika kwa jina la Frednand Laulian amefanikisha utafiti wake uliomwezesha kukusanya zana mbalimbali na kuzitumia kutengeneza pikipiki isiyotumia petrol akiwa na kusudio la kusaidia jamii kukabiliana na ongezeko la bei ya nishati ya mafuta pamoja na mabadiliko ya tabianchi.

Bw. Laulian anabainisha kuwa hakuwa akifurahishwa na namna ya mafuta ya petrol yanavyopanda bei kila kukicha na kusababisha kuongezeka kwa bei ya bidhaa nyingine na ugumu wa Maisha na akaamua kubuni pikipiki ambayo haitumii mafuta

Ujuzi huu wa Frednand unafanikiwa wakati dunia ikipambana dhidi ya mabadiliko ya tabia nchi, moja ya mikakati ya kimataifa ni kupunguza uzalishaji na utumiaji wa hewa ukaa kutoka kiwandani na katika vyombo vya usafiri ikiwemo magari na pikipiki vinavyotumia mafuta.

Jitihada za dunia zinalenga kupunguza matumizi ya dizeli na petrol na baadala yake gesi na nishati nyingine za umeme zinapigiwa upatu, Laulian ni mmoja wa wabunifu ambao wakitumika ipasavyo watakuwa na mchango mkubwa katika ukuaji wa sekta ya viwanda na teknlojia nchini Tanzania ingawa anakabiliwa na changamoto kadhaa

Wabunifu wengi na watu wenye ujuzi wa fani mbalimbali hukwama kutokana na kukosa uungwaji mkono kutoka kwa wadau na hata taasisi za umma, serikali na mashirika ya kimataifa, Laulian ni mmoja wa wajuzi wanaokumbana na mkwamo wa malezi ya kiufundi, mitaji na nyezo

Jamii katika Kijiji chake inavyomtafsiri vipi kijana Kijana Frednand Laulian ambaye tayari amefanikiwa kuuza pikipiki yake kwanza aliyoitengeneza mwaka jana huku nyingine ikifikia asilimia 95?

Yustus Robert Mkazi wa Ruyenzi Kakonko anasema kwa kipindi alichomfahamu, Frednand amekuwa akibuni zana mbalimbali kiasi cha kuwavutia vijana wengi kujiunga na karakana yake ili kujifunza fani mbalimbali na kwamba hata yeye ni mwanafunzi wake

Bw. Wenceslaus Rafael Mkazi wa Kabingo – anashuhudia kuwa mbunifu huyo amekuwa msaada katika Kijiji chake tanhu alipomaliza masomo ya ufundi katika chuo cha zamani cha Ufundi Kakonko na anatoa wito kwa mamlaka za serikali kumsaidia kupata ujuzi zaidi Pamoja na mtaji.

Tanzania inao wabunifu wengi nje ya mfumo rasmi wa elimu na taasisi za ufundi ambao kila mwaka huibuliwa wakiwa na bunifu mbalimbali za matumizi ya zana zilizopo katika shughuli za kisayansi na kiufundi ambao hata hivyo wanakosa usaidizi wa mafunzo na mitaji kama ilivyo kwa Frednand Laulian

Mwandishi: Prosper Kwigize

Mhariri: Adela Madyane

 

Post a Comment

0 Comments