Uchaguzi Utakuwa Huru na wa Haki – Samia

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan amesema haki, demokrasia, sheria na utawala bora utadumishwa kwa watu wote wakati wa Uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika mwaka huu.

 

Rais Samia amesema hayo leo katika sherehe za mwaka mpya 2024 (Diplomatic Sherry Party) kwa Mabalozi wanaoziwakilisha nchi zao hapa nchini pamoja na wawakilishi wa mashirika ya kimataifa zilizofanyika Ikulu.  

 

Aidha, Rais Samia amesema ili kuhakikisha uchaguzi huru na wa haki, Kikosi Kazi huru cha kupitia na kushauri mageuzi muhimu katika mfumo wa siasa kiliundwa ambapo kiliwasilisha ripoti yake mwaka 2023.

 

Rais Samia pia amesema mapendekezo mengi ya Kikosi Kazi yaliyopokelewa na serikali na wadau wote yalihusu kuongeza uwazi katika michakato ya uchaguzi ikiwa ni pamoja na uteuzi wa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi.

 

Vile vile, Rais Samia amesema masuala machache hayakupokelewa moja kwa moja ambayo yalikuwa kinyume na katiba hivyo yanaweza kuchukuliwa wakati wa mchakato wa marekebisho ya katiba.

 

Rais Samia amesema serikali itaendeleza ushirikiano na balozi hizo kwa mujibu wa katiba, tunu za kitaifa, usawa, umoja na mshikamano wa kitaifa huku akiwataka mabalozi hao kutokuingilia uchaguzi na kuzingatia mila, kanuni na maadili ya kidiplomasia.

 

Kwa upande mwingine, Rais Samia amesema Tanzania inasikitishwa na vita vinavyoendelea Palestina na kusababisha mauaji ya watoto na raia wasio na hatia na inaunga mkono usuluhishi kati ya Palestina na Israeli kwa kutoa wito wa kusitishwa mapigano na kupatiwa misaada ya kibinadamu.

Post a Comment

0 Comments