Mwassa awapa somo Wahitimu Vyuo vya Ualimu kujitolea

Wahitimu wa mafunzo ya Ualimu katika chuo cha Ualimu Katoke Daraja A kilichopo wilayani Muleba mkoani Kagera  wamehimizwa kuomba nafasi za kujitolea katika maeneo yao wakati wakisubiri ajira na kutokukubali kukaa nyumbani bila kuwa na kazi yoyote ya kufanya .

Mkuu wa mkoa wa Kagera Fatuma  Mwassa amesema hayo wakati wa Maafali ya 85 ya chuo cha ualimu katoke kwa wanafunzi wa mafunzo ya ualimu daraja A yaliyofanyika chuoni hapo April 25.

Mh Mwassa amesema kuwa mkoa huo utatoa fursa za kujitolea kwa wanafunzi waliohitimu   mafunzo ya Ualimu kujitolea kufundisha  katika shule zilizopo mkoa wa Kagera hivyo wanafunzi hao hawatakiwi kukaa nyumbani kuosha  vyombo na kusaidia kupika badala yake wajishughulishe katika shughuli mbalimbali 

Mkuu wa mkoa wa Kagera Fatuma Mwassa wakati akizungumza na wahitimu wa mafunzo ya Ualimu daraja A chuo cha Ualimu Katoke

Amesema kuwa kwa wale ambao hawatokuwa kwenye fursa za kujitolea wanaweza kufungua biashara ndogo ndogo za Mpesa na ujasiriamali kwani wakati wako chuoni wamefundishwa ni kwa jinsi gani wanaweza kujikwamua kiuchumi ili waweze kuingiza kipato hata kidogo badala ya kutegemea wazazi

Kwa upande wake mkuu wa chuo hicho Bwana Michael Ntwale  ameiomba serikali kuwatatulia changamoto ya ukosefu wa nishati mbadala amesema kuwa licha ya  kuwa ukatikaji wa umeme kutokuwa  wa mara kwa mara kama ilivyokuwa awali lakini wakiwa na nishati mbadala itawasaidia wanafunzi wa chuo hicho inapotokea umeme ukakatika .

Mkuu wa mkoa wa Kagera Fatuma Mwassa akitoa vyeti kwa wahitimu wa mafunzo ya Ualimu chuo cha Ualimu Katoke

Naye Emmanuel Jonas wakati akisoma Risala kwa niaba ya wahitimu hao amesema kuwa walianza masomo yao mwaka 2022 wakiwa wanafunzi 202 lakini waliohitimu ni 198 na wengine 4 waliondoka chuoni kutokana na sababu mbalimbali.

Aidha amesema kuwa licha ya mafanikio zipo changamoto mbalimbali ambazo wangeomba serikali kuzitatua ikiwa ni pamoja na ukosefu wa nishati mbadala kwa ajili ya kujisomea pindi umeme unapokatika, uchakavu wa nyumba na makazi wanayoishi watumishi wa chuo pamoja na uchakavu wa mashine ya kusambaza maji kwenye chuo hicho.

Mkuu wa chuo cha Ualimu Katoke Michael Ntwale akizungumza wakati wa mahafari ya 85 tangu kuanzishwa kwa chuo hicho

Mwandishi: Mariam Kagenda
Mhariri: Prosper Kwigize



Post a Comment

0 Comments