THPS yapeleka neema kwa wenye VVU tarafa ya Ilagala

 

Shirika la Tanzania Health Promotion Support (THPS) limetumia kiasi cha Sh.270 milioni kwa kituo cha afya cha Ilagala, wilayani Uvinza mkoani Kigoma, kwa ajili ya ukarabati wa jengo la kliniki ya tiba na matunzo kwa wenye virusi vya UKIMWI, pamoja na vifaa tiba na samani.

Hafla ya makabidhiano ya jengo hilo imefanyika jana katika Kituo cha Afya cha Ilagala, ambapo Mkurugenzi wa Miradi wa Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa cha Marekani (U.S. CDC )Tanzania, Dkt. George Mgomella akiambatana na Mkurugenzi Mtendaji wa THPS, Dkt. Redempta Mbatia wamekabidhi jengo hilo, samani na vifaa vya uchunguzi na kinga ya saratani ya mlango wa kizazi kwa Mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Mhe. Thobias Andengenye aliyewakilishwa na mganga mkuu wa Mkoa Dkt. Jesca Lebba.

Ukarabati huo uliogharimu jumla ya Shilingi milioni 211, ulihusisha urekebishaji wa vyumba mbalimbali vya matibabu ndani ya jengo hilo, vikiwemo vyumba vya ushauri nasaha, chumba cha usajili, maabara, chumba cha kutolea dawa, sehemu ya kusubiria huduma na chumba cha kutunza kumbukumbu za matibabu.

Dr. Mgomella alibainisha kuwa uboreshaji wa jengo hilo pamoja na vifaa tiba ambao umefanyika kwa ufadhili wa Mpango wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kukabiriana na UKIMWI (PEPFAR) na U.S. CDC kupitia mradi wa Afya Hatua unaotekelezwa na Shirika la THPS, utasaidia kuwepo kwa mazingira mazuri zaidi ya utoaji wa huduma bora za afya hususani tiba na matunzo kwa wapokea huduma wenye maambukizi ya virusi vya UKIMWI.

Dkt. George Mgomella Mkurugenzi wa Miradi wa U.S. CDC Tanzania akihutubia wakati wa hafla ya kukabidhi jengo la CTC, katika kituo cha Afya Ilagala, wilayani Uvinza 


Dkt. Mgomella alisisitiza umuhimu wa ushirikiano katika mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI huku akipongeza Wizara ya Afya, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, viongozi wa mkoa wa Kigoma, mamlaka za serikali za mitaa na Shirika la THPS kwa dhamira yao thabiti ya kutoa huduma bora za afya kwa wananchi.

"Ukarabati uliofanyika, sio tu utaboresha huduma zinazotolewa lakini pia mazingira ya kutolea huduma yatavutia jamii kufika na kupata huduma katika kituo hiki", alisema Dr. Mgomela.

Jengo la huduma na matunzo kwa wenye maambukizi ya VVU lililokarabatiwa na THPS katika kituo cha afya Ilagala mkoani Kigoma


Sambamba na jengo lililofanyiwa ukarabati, CDC na THPS pia walikabidhi mashine tatu za Thermocoagulation na zingine tatu za Cryotherapy ili kusaidia utambuzi na matibabu na kuzuia saratani ya mlango wa kizazi kwa wasichana mkoani Kigoma.

Mashine hizo, zenye thamani ya jumla ya Sh. 58.7 milioni zitasaidia katika kutoa huduma na kuokoa maisha kwa wanawake waliopo katika eneo hilo na kusaidia utekelezaji wa mpango wa taifa wa kupambana na saratani ya mlango wa shingo la kizazi.

"Tunaamini kwamba kwa kuwekeza katika teknolojia hizi za kiwango cha juu, tunaweza kuchangia katika kuokoa maisha wa walengwa", alisema Dkt. Mgomella.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa THPS Dkt Redempta Mbatia amepongeza uwepo wa sera nzuri za afya ndani ya Serikali ya Tanzania akieleza kuwa sera hizo ndizo zimechochea serikali ya Marekani kutoa ufadhili mkubwa katika miradi ya afya nchini Tanzania.

“Tukumbuke kuwa kama sio sera Madhubuti za Serikali yetu, hata ufadhili huu tusingeupata”, alisema Dkt. Mbatia.

Dkt Redempta Mbatia Mkurugenzi wa THPS Tanzania akitoa taarifa ya utekelezaji wa mradi wa ukarabati wa kliniki ya CTC Ilagala

Dkt. Mbatia alibainisha kuwa kupitia mradi wa Afya Hatua THPS inatoa huduma za afya za kinga na matibabu kwa wenye maambukizi ya virusi vya ukimwi katika vituo 67 vya afya mkoani Kigoma.

Alieleza kuwa pamoja na huduma za kinga, na tiba THPS imewezesha mkoa kuajili watumishi wapatao 262 ambapo kati yao 22 wameajiriwa katika Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Kigoma, na kwamba tangu mwaka 2011 THPS na serikali ya mkoa wa Kigoma wamewafikia watu wenye virusi vya Ukimwi 51,757 ambapo 22,086 kati yao wapo kwenye matibabu ya VVU na 99% wamefubaza virusi vyao.

Wananchi pamoja na wahudumu wa afya Ilagala wakifuatilia kwa umakini hafla ya makabidhiano ya jengo la kliniki ya huduma za mapambano ya virusi vya Ukimwi katika kituo cha afya Ilagala

Hata hivyo Dkt Mbatia ametahadharisha kuwa pamoja na kwamba jitihada hizi zimesaidia kupunguza maambukizi ya VVU katika mkoa wa Kigoma hadi 1.7% ukilinganisha na mwaka 2017 ambapo maambukizi yalikuwa 2.9%, bado kuna idadi kubwa ya vijana ambao hawajitokezi kupima afya zao.

Akizungumza katika hafla hiyo mkuu wa mkoa wa Kigoma Mhe. Andengenye kupitia katika hotuba yake iliyosomwa na mganga mkuu wa mkoa wa Kigoma Dkt. Jesca Lebba alitoa shukrani zake za dhati kwa msaada unaotolewa na serikali ya Marekani kupitia CDC na THPS katika mapambano dhidi ya janga la UKIMWI mkoani Kigoma. 

Mhe. Andengenye aliahidi kudumisha ushirikiano na CDC na THPS ili kuendelea kuokoa maisha na kudhibiti VVU na UKIMWI katika mkoa huo. Mhe. Andengenye alipongeza ushirikiano na jitihada kubwa za wadau katika vita dhidi ya VVU. 

Dkt. Jesca Leba Mganga mkuu wa mkoa wa Kigoma akihutubia wananchi, wataalamu na wafadhili kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Kigoma

“Kituo hiki ni muhimu sana katika kutoa huduma za afya katika eneo hili, na naamini kuwa maboresho yaliyofanyika yataongeza motisha kwa wahudumu wa afya katika kuhudumia jamii yetu", alisema.

Mradi wa CDC/PEPFAR Afya Hatua ni uthibitisho wa juhudi za ushirikiano za wadau wa ndani na kimataifa wanaohusika katika utekelezazi wa afua mbalimbali zinazolenga kusaidia upatikanaji wa huduma bora za afya. 

“Naomba mhakikishe kituo hiki na vifaa vilivokabidhiwa vinatumika ipasavyo na kutunzwa vizuri, ili kuhakikisha kuwa wananchi wa eneo hili wanaendelea kupata huduma bora za afya, na pia kuweza kuzuia ipasavyo saratani ya mlango wa kizazi na hivo kuokoa maisha,” alisema.

Pamoja na shukurani hizo, Mhe. Andengenye ameomba THPS kuendelea kusaidia juhudi za serikali za kuporesha huduma za afya ikiwemo kuanzisha huduma za tiba na matunzo kwa wenye VVU katika zahanati za Businde, Msufini na Rungwe mpya sambamba na kutoa mafunzo kwa wahudumu wapya wa afya kuhusiana na kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto. 

Kutoka kushoto ni Dkt. Jesca Leba Mganga mkuu wa mkoa wa Kigoma, Dkt. George Mgomella Mkurugenzi wa Miradi wa U.S. CDC Tanzania na Dkt. Redempta Mbatia mkurugenzi wa THPS wakifurahia baada ya kufungua bango lengye maelezo ya makabidhiano ya jengo la CTC kituo cha Afya Ilagala, wilayani Uvinza 

Baadhi ya wananchi waliohudhuria hafla hiyo walikiri kuwa eneo lao limekuwa na uhitaji mkubwa wa huduma za CTC kutokana na jiografia yake ambapo walilazimika kuifuata huduma hiyo zaidi ya kilimota 100 kwenda Hospitali ya wilaya iliyoko makao makuu ya wilaya ya uvinza

Hassan Nona na Zuwena Abubakar ambao ni wakazi wa Ilagala wameiambia Buha News kuwa kutokuwepo na kituo cha kisasa cha CTC kulipelekea waliobainika kuwa na maambukizi kukosa hudama bobevu na kupelekea wengi wao kuacha kuhudhuria kituoni hapo

"Kutokana na huduma kupatikana mbali na eneo letu wapo wanaoishi na VVU walioamua kujificha au kusitisha kupata huduma zinazotakiwa lakini kwa ukarabati huu uliofanywa na THPS pamoja na vifaa ambavyo vimewekwa tuna imani kuwa watu wengi zaidi watajitokeza kupima na watakaokutwa na maambukizi watapata huduma" alisisitiza Zuweza 

Kwa upande wake Hassan Nona alitumia fursa hiyo kutoa wito kwa vijana kujitokeza kupima afya zao na kuepuka tabia ya kuwaweka wanawake kama kinga kwao kukwepa kupima na kutekemea majibu ya vipimo vya wake zao wanapokuwa na ujauzito 

Dkt. Jesca Leba (kulia) akipokea sehemu ya vifaa vilivyotolewa kwa ajili ya kupima magonjwa hususani Saratani ya mlango kwa kizazi kwa wanawake 

Katibu Tawala wa Mkoa wa Kigoma, Mganga Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya ya Uvinza, Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya Wilaya ya Uvinza, Mganga Mkuu wa Wilaya, Watumishi wa Kituo cha Afya Ilagala, Maafisa wa THPS na wananchi wa Uvinza walihudhuria na kushuhudia tukio hilo muhimu.

Kuhusu THPS

Tanzania Health Promotion Support (THPS) ni asasi isiyo ya kiserikali iliyoanzishwa mwaka 2011, chini ya Sheria ya asasi zisizo za kiserikali nambari 24 ya 2002. 

THPS inafanya kazi kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania kupitia Wizara za Afya za Tanzania Bara na Zanzibar; Wizara ya Jinsia, Vijana, Wazee na Makundi Maalum; Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Kwa ufadhili wa Mpango wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Misaada ya UKIMWI kupitia Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa, THPS inatekeleza afua mbalimbali za VVU/UKIMWI; Kifua kikuu; kuzuia ukatili wa kijinsia dhidi ya watoto; huduma za afya ya uzazi, uzazi, watoto wachanga, watoto na vijana; mifumo ya habari ya maabara na usimamizi wa afya, na UVIKO-19. 

Wananchi wa Ilagala na watumishi wa sekta ya afya wakishuhudia uzuri wa jengo la huma za afya kinga na tiba kwa wenye Virusi vya Ukimwi katika kituo cha afya Ilagala lililokarabatiwa kwa hisani ya watu wa marekani kupitia mfuko wa dharua wa Rais wa Marekani, CDC na THPS

Kliniki ya Tiba na Matunzo ya Kituo cha Afya cha Ilagala wilayani Uvinza, Kigoma imefanyiwa marekebisho makubwa kupitia mradi wa Afya Hatua unaotekelezwa na Shirika laTanzania Health Promotion Support (THPS) kwa ufadhili wa Mpango wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kudhibiti UKIMWI (PEPFAR), kupitia Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa cha Marekani (U.S. CDC). 

Kuhusu mradi wa CDC/PEPFAR Afya Hatua (Oktoba, 2021- Septemba, 2026)

Mradi huu unalenga kutoa huduma jumuishi katika vituo vya afya (Kigoma, Pwani, Shinyanga na Tanga) na katika jamii (Kigoma, Pwani na Tanga).

Huduma hizi ni pamoja na matibabu na matunzo ya watu wanaoishi na VVU, huduma za kitabibu za tohara kwa wanaume katika mikoa ya Kigoma na Shinyanga na programu ya DREAMS kwa wasichana balehe na wanawake wadogo katika mkoa wa Shinyanga.

Mwandishi: Prosper Kwigize

Mhariri: Adela Madyane

Post a Comment

0 Comments