USAID yazindua mradi wa mpango wa lishe bora mkoani Kigoma

Jumla ya watoto milioni 1.2 wenye umri wa chini ya miaka mitano watafikiwa na mradi wa lishe ikiwa ni jitihada za kukabiliana na changamoto ya udumavu katika mikoa ya Njombe, Songwe, Rukwa, Katavi na Kigoma.

Hayo yamesemwa na mkurugenzi wa mradi wa lishe Joyceline Kaganda katika hafla ya uzinduzi wa Mradi wa mpango jumuishi wa Lishe unaofadhiliwa na shirika la kimataifa la Maendeleo la Marekani (USAID) uliofanyika jana mkoani Kigoma, mradi ambao unaotekelezwa kwa miaka mitano kuanzia Oktoba 2023 - Septemba 2028.

Amesema Mradi huo  unagharimu jumla ya Dola za Kimarekani milioni 40 na unatarajiwa kuleta mabadiliko katika afya za watoto na wanawake ambao mpaka sasa wanakabiriwa na utapiamlo kwa asilimia 30.

Mradi unalenga kuangalia mambo mbalimbali ikiwemo ubora wa huduma za lishe kwenye vituo vya afya, upatikanaji wa maji safi na salama, ulaji wa chakula chenye virutubisho na kuongeza uwezo wa halmashauri katika matumizi ya takwimu.

“Mradi unatarajia pia kutoa elimu juu ya mabadiliko ya tabia ya namna ya uandaaji wa chakula cha mtoto, elimu ambayo itakuwa inatolewa katika siku ya afya ya kijiji ambapo wanawake wataelekezwa namna ya kuandaa chakula hicho kwaajili ya kupata afya bora” almesema Kaganda.

Mkurugenzi mkuu wa idara ya Lishe kutoka shirika la umoja wa mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF) Patric Codjia akiwawakilisha wadau wa Lishe nchini amesema takwimu za sensa za mwaka 2022, zinaonesha jitihada za serikali za kupunguza udumavu licha ya kuwepo kwa changamoto ya matumizi mabaya ya  chakula ikiwa ni moja ya sababu kuu ya udumavu ikiendelea kuwepo katika mikoa hiyo.

Viongozi kutoka USAID pamoja na sekretaieti ya mkoa wa Kigoma wakiangalia moja ya kitalu darasa cha mbogamboga mjini Kigoma

Codjia amesema harakati za kupunguza udumavu katika mikoa hiyo zinakwenda taratibu na kwamba ili kuondokana na changamoto hiyo elimu ya kina inatakiwa itolewa kwa wanawake wajawawzito juu ya namna ya  kuziishi siku 1000 za ujauzito na ukuaji wa mtoto.

“Wanawake wengi wanakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa chakula bora, wengine wanapata chakula cha msimu, wengine hawana ufahamu wa lishe bora ya utotoni na wengine wanapata changamoto namna ya kufika katika kliniki zenye huduma ya lishe, yote haya yanasababiaha udumavu, tunaamini kupitia mradi wa USAID Lishe tutafanya kazi kwa ushirikiano wa karibu na serikali za mitaa na sekta binafsi kutatua changamoto hizo” Amesema Codjia

Naye Eliuta Kivele mwakilishi kutoka ofisi ya Waziri mkuu amesema mradi huu ni muhimu kwakuwa unaandaa watu ambao watakuwa tayari kushiriki katika maendeleo ya nchi na kwamba utachangia katika utekelezaji wa mpango jumuishi wa utekelezaji wa afya na lishe kwa kipindi cha miaka mitano kuanzia 2021/2026.

Pia, amesema mradi huu utachangia katika utekelezaji wa dira ya maendeleo ya mwaka 2025 na mpango wa maendeleo wa taifa wa miaka mitano 2021/2026 ambao moja ya maeneo ya mkazo ni kushughulikia suala la lishe.

Maonesho ya baadhi ya vyakula lishe vinavyopendekezwa kuliwa kwa ajili ya afya kwa binadamu

Hata hivyo Craig Hart mkurugenzi wa misheni kutoka USAID amefurahishwa na matokea ya ufadhili wanaoutoa kwa nchi ya Tanzania kwa kutoa matokea chanya katika afya akitoa mfano wa namna umri wa kuishi wa Watanzania ulivyoongezeka kwa miaka 15 kuanzia mwaka 2000-2019 kupitia miradi ya afya yenye lengo la kuokoa maisha.

“Kwa kipindi cha miaka 20 iliyopita, USAID  imetoa dola bilioni 7.5 katika sekta ya afya nchini, tunajivunia kuona serikali ya Marekani inaendelea kuwa kinara katika kuhudumia jamii kwa kubadili afya za watanzania na zaidi kulingana na matokeo chanya ya kuokoa maisha ya watu” amesema Hart. 

Akizungumzia upande wa lishe Hart amesema kwa kipindi cha miaka 10, wamewekeza jumla ya dola million 600 katika sekta ya lishe na kuwataka viongozi wa mikoa wanaotekeleaa mradi wa lishe kujifunza namna Morogoro, Iringa na Manyara walivyoweza kuounguza changamoto ya udumavu kati ya asilimia 35-49 ili nao wapate matokea tarajiwa kwaajili ya mradi

Mwandishi: Adela Madyane

Mhariri: Prosper Kwigize 

Post a Comment

0 Comments