Serikali ya Tanzania inatarajia kukihamisha Kijiji cha Katoto kilichopo ndani ya bonde la mto Malagarasi wilayani Kasulu ili kupisha uhifadhi wa bonde la ardhi oevu na ramsa ya Mto Malagarasi ambao uko hatarini kutoweka kutokana na uvamizi wa wakulima na wafugaji
Azimio hilo la Baraza la
Mawaziri limewasilishwa na mkuu wa wilaya ya Kasulu Kanali Isack Mwakisu wakati
akihutubia Baraza la madiwani la halmashauri ya wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma
Akinukuu maagizo ya Baraza la
Mawaziri Kanali Mwakisu amebainisha kuwa wakazi wa Katoto ambao ni wafugaji
watapewa ardhi mpya jirani na kijiji cha Kagerankanda katika eneo la sehemu ya
kitalu cha uwindaji ili kuanzisha makazi mapya.
“Baada ya tafakari ya muda mrefu
inayoenda sambamba na kubaini athari za mabadiliko ya tabia nchi yanayoukabiri
mto malagarasi ambao unachangia asilimia 70 ya maji yanayoingia katika ziwa Tanganyika,
serikali sasa itakihamisha kijiji cha Katoto ili kupisha uhifadhi wa ramsa ya
bonde la Malagarasi ambayo inatambuliwa kimataifa” Alisisitiza Kanali Mwakisu
Mpaka wa Wilaya za Kasulu na Uvinza kuhakikiwa ili kuondoa migogoro ya ardhi na mgongano wa maslahi baina ya halmashauri hizo. Lengo ni kuweka mipaka rasmi na kuwezesha usimamizi sahihi wa maliasili (maji na misitu)
— BUHA FM RADIO (@FmBuha) May 9, 2024
DC Kasulu Kanali Isack Mwakisu awatangazia Madiwani Kasulu DC pic.twitter.com/ifLHP8zmev
Mkuu huyo wa wilaya amewataka
madiwani na viongozi wa serikali katika halmashauri hiyo kutoa ushirikiano
katika utekelezaji wa azimio la kukihamisha kijiji hicho huku akibainisha kuwa
taratizo zitakapokamilika wananchi wa kijiji hicho wataarifiwa na kuandaliwa
kwa ajili ya kuhama.
Wakati huo huo Mkuu wa wilaya ya
Kasulu amewatangazia wananchi wa wilaya hiyo kuwa serikali inatarajia kuhakiki
na kupima mipaka ya ardhi na hifadhi ya misitu katika wilaya hiyo ili kumaliza
migogoro ya ardhi baina ya wakulima, wafugaji na serikali
Akihudubia katika baraza la
madiwani Kanali Mwakisu amebainisha kuwa kumekuwepo na migogoro ya muda mrefu
inayotokana na wananchi kuvamia ardhi katika hifadhi za misitu katika eneo la Kagerankanda
na Mvinza pamoja na eneo la Makere kusini na Kaskazini hali inayosababisha uharibifu
mkuwa wa mazingira.
“Tunatambua kuwa lipo tatizo
kubwa la migogoro ya aridhi inayotokana na kutofahamika kwa mipaka rasmi katika
maeneo ya hifadhi na vijiji, hivyo serikali imeandaa utaratibu wa kuhakiki
mipaka na pia kupima upya baadhi ya maeneo yenye migogoro” Amesema kanali
Mwakisu
Amebainisha kuwa licha ya
wakulima kupewa ardhi yenye ukubwa wa hekta 10000 na aliyekuwa Rais wa jamhuri
ya muungano wa Tanzania hayati Dr. John Magufuli wananchi wameendelea kuingia
na kufanya shughuli za kibinadamu katika maeneo yasiyoruhusiwa na kusababisha
migogoro
Kuhusu wananchi waliolima ndani
ya hifadhi za misitu kuomba kibali cha kuvuna mazao yao, kanali Mwakisu
amebainisha kuwa hana mamlaka ya kutoa kibali cha kufanya hivyo, huku
akiwashangaa wananchii ambayo waliingia kinyemela hifadhini kulima bila vibali na
sasa wanaomba kibali kwenda kuvuna
Kufuatia kuwepo kwa zuio la
kisheria kwa mwananchi yeyote kutoruhusiwa kuingia katika hifadhi za taifa,
kanali Mwakisu amewataka madiwani kutoa elimu kwa wapiga kura wao na kuepuka
kuwachonganisha na serikali.
Madiwani katika halmashauri hiyo
wamemhakikishia mkuu huyo wa wilaya kutoa ushirikiano wa dhati kwa kuwaelimisha
wananchi kutovunja sharia za ardhi na hifadhi za misitu.
Mwandishi: Prosper Kwigize
Mhariri: Adela Madyane
0 Comments