Tanzania inapoteza hekta 469,000 kila mwaka kutokana na uharibifu wa mazingira

 

Shirika la Umoja wa mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR mkoani Kigoma, limeongoza maadhimisho ya siku ya kimataifa ya mazingira maarufu kama Siku ya Mazingira duniani kwa kuhamasisha utunzaji wa mazingira katika kambi za wakimbizi mkoani Kigoma

Maadhimisho hayo yamefanyika katika Kambi ya wakimbizi mseto ya Nyarugusu wilayani Kasulu, wakati dunia ikiadhimisha siku ya mazingira, mataifa mbalimbali yanakabiriwa na changamoto nyingi za athari za mabadiliko ya tabia nchi hali inayopelekea uharibifu wa ardhi na bayonuai kote ulimwenguni na kuamsha ari ya kila nchi kuweka mikakati ya kupunguza athari hizo.

Akihutubia katika maadhimisho hayo Mkuu wa wilaya ya Kasulu Kanali Isack Mwakisu ambaye alikuwa mgeni rasmi ameweka bayana kuwa Tanzania ni miongoni mwa nchi zinazoshuhudia uwepo wa athari za kimazingira ikipoteza zaidi ya hekta 469,000 za misitu kila mwaka sambamba na bayonuai mbalimbali

Kanali Mwakisu amebainisha kuwa ili kukabiliana na athari hizo juhudi za makusudi na za pamoja lazima zifanyike ikiwa ni pamoja na kupanda miti na kulinda vyanzo vya maji

Mkuu wa wilaya ya Kasulu Kanali Isack Mwakisu (kulia) akitembelea maonesho ya shughuli za mazingira katika Kambi ya wakimbizi Nyarugusu. Picha na. Maimuna Mtengela


Kwa upande wake mkuu wa ofisi ya shirika la kuhudumia wakimbizi UNHCR wilayani Kasulu Bw. Jean Bosco Ngomoni amekiri kuwa shirika hilo linatambua uwepo wa uharibifu wa mazingira unaotokana na shughuli za kuwahudumia wakimbizi katika kambi zao na kwamba Umoja wa mataifa pamoja na wadau wake wanahakikisha kuwa mazingira yanahifadhiwa na kurejeshwa katika uasili wake

Afisa mazingira wa UNHCR Bw. Godfrey Oyema amebainisha kuwa Umoja wa unatambua umhimu wa kutunza mazingira, na kwamba shughuli za upandaji miti zinapewa kipaumbele kwa kushirikisha jamii ya wakimbizi na wenyeji.

“Tunaishukuru sana serikali ya Ubelgiji, imetupatia pesa za kutosha kwa ajili ya mradi wa mazingira na madiliko ya tabia nchi, na UNHCR kwa kushirikiana na wadau, wakimbizi na wenyeji tayari tumeshapanda miti ipatayo milioni sita na kwa ujumla mazingira yako vizuri” Amesisitiza Oyema.

Kaimu mkuu wa kambi ya wakimbizi mseto ya Nyarugusu inayohifadhi raia wa Burundi na DRC Bw. Hamphrey Mrema amekiri kuwa kutowapatia wakimbizi nishati mbadala ya kupikia ndiyo chanzo cha uharibifu wa mazingira katika kambi hiyo huku akipongeza shirika la umoja wa mataifa la kuhudumia wakimbizi kwa kutoa fedha kwa ajili ya kunusuru mazingira

Kauli mbiu ya maadhimisho ya siku ya mazingira duniani mwaka huu ni “Ardhi yetu ndiyo kesho yetu.

Mwandishi: Prosper Kwigize

 

 

Post a Comment

0 Comments