Mbunge wa Jimbo la Kasulu mjini Profesa Joyce Ndalichako amemshukuru Rais Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha za kutosha kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo katika jimbo la Kasulu katika kipindi cha miaka minne iliyopita.
Shukurani hizo amezitoa katika mkutano wa hadhara wa wananchi uliofanyika jana katika kata ya Mwilamvya mjini Kasulu ambao ni sehemu ya ziara ya kutembelea na kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika kata zote za jimbo hilo.
Prof. Ndalichako ametaja miradi mikubwa iliyotekelezwa katika jimbo hilo tangu alipochaguliwa kuwa mbunge kuwa ni pamoja na ujenzi wa shule za sekondari kumi mpya, shule za msingi 5, vituo vya afya viwili oamoja na zahanati katika kata za Kumyika, Mwilamvya na Msambara.
Kuhusu miradi ya Maji, Prof. Ndalichako amebainisha kuwa moja ya kata zilizokuwa zikikabiliwa na tatizo kubwa la maji ni pamoja na kata ya Kigomdo mtaa wa Nyachijima, Nyarumanga na Kidyama ambao kwa miaka zaidi ya 30 waliishi bila huduma ya maji ya uhakika na sasa tayari mradi wa maji wa Nyachijima umekamilika na kuanza kutoa huduma.
Maeneo mengine ya miradi ya maji ni pamoja na Mudyanda, Murubona, Muganza, Mwanga, Msambara na Mwilamvya ambapo pamoja na mradi mkubwa wa Maji wa Mwanga, tayari serikali imetoa kiasi cha shilingi bilioni 35 kwa ajili ya mradi wa maji wa mjini Kasulu ambao utasambaza maji katika kata zote.
Profesa Ndalichako ameeleza kuwa, Rais Dkt. Samia ni msikivu na kwamba klila maombi ambayo amekuwa akipelekewa na wabunge wa mkoa wa Kigoma anayashughulikia haraka na pesa zinatolewa ili kuwarahisishaia wananchia wa mkoa wa Kigoma kupata maendeleo ya haraka
Miradi mingine ambayo Jimbo la Kasulu linajivunia ni ujenzi wa barabara kuu kutoka kabingo hadi manyovu, kilomita 1.9 za lami katika kata ya Murubona na uchongaji wa barabara za mitaani mjni Kasulu ikiwemo kata ya Mwilamvya.
Naye Diwani wa Kata ya Mwilamvya Mh. Emmanuel Gamuye amemshukuru Mbunge wa Kasulu Mjini Prof. Joyce Ndalichako kwa namna alivyosaidia kata hiyo kupata fedha za kutekeleza miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa zahanati, na shule mpya ya msingi Mwilamvya na shule ya sekondari Mwilamvya mpya.
Mh. Gamuye amebainisha kuwa licha ya uchanga wake Kata ya mwilamvya ni kata kubwa yenye idadi kubwa ya watu na watoto wanaosoma elimu ya msingi hivyo ili kuwahudumia kimalezi na kielimu mchakato wa wa ujenzi wa shule nyingine ya msingi unaendelea.
Mamia ya wananchi hususani wanawake walijitokeza kumlaki mbunge wao huku wakitoa shukurani zao kwa Rais kwa kusikiliza maombi yao kupitia kwa mbunge wao.
0 Comments