Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ameiagiza
Wizara ya Kilimo kuisimamia kwa ukaribu Sekta ya Ushirika ili uwekezaji unaofanywa na
Serikali kwenye sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi uweze kufanywa na Vyama vya Ushirika.
Rais Samia ametoa agizo hilo leo katika kikao na Maafisa Ugani na wanaushirika
kilichofanyika Ikulu, Chamwino.
Aidha, Rais Dkt. Samia amesema Serikali ina dhamira ya kurudisha hadhi ya ushirika
hususan ushirika wa mazao hivyo ametaka Ushirika uendeshwe kisasa, uwekezaji ufanywe
kitaalam na ukiwa na lengo la kumnufaisha mwanaushirika moja kwa moja.
Vile vile, Rais Dkt. Samia amevitaka Vyama vya Ushirika kutokuwa sehemu ya kumyonya
mwanaushirika, bali viwe mstari wa mbele kuwalinda na kuwatetea.
Rais Dkt. Samia pia amevielekeza Vyama vya Ushirika kuwa chachu ya mabadiliko na
vyenye kuleta mageuzi ya fikra, ikiwemo kuchangia maendeleo mapana kwa kuhamasisha
wanaushirika waweze kujiunga na mifuko ya hifadhi ya jamii na Mfuko wa Bima ya Afya kwa
wote.
Rais Dkt. Samia ameagiza Maafisa Ugani na Maafisa Ushirika kuhakikisha kuwa ruzuku ya
pembejeo inayotolewa na Serikali inaleta matokeo makubwa zaidi, kuwafikia wananchi vijijini
pamoja na kuwaelimisha mbinu bora za kilimo, ufugaji na uvuvi.
Kwa upande mwingine, Rais Dkt. Samia ameitaka Wizara ya Kilimo kuandaa utaratibu wa
kuwapima Maafisa Ugani kwa tija inayozalishwa kwenye Kata au Kijiji anachokisimamia ili
uwekezaji unaoufanywa na Serikali utoe matokeo yanayotarajiwa.
Hali kadhalika, Rais Dkt. Samia amewataka Maafisa Ugani katika ngazi ya Kata kukaa
kwenye vituo vyao na kutumia usafiri ambao Serikali imewapatia kuwafikia na kuwahudumia
wananchi.
Rais Dkt. Samia ameeleza kuwa Serikali itaunga mkono juhudi za wanaushirika kuanzisha
Benki ya Ushirika ya Taifa kwa kuchangia Shilingi Bilioni 5 kama mtaji ili kuwezesha shughuli
za Benki hiyo kuanza.
0 Comments