Kiongozi wa Chama cha Wiper, Kalonzo Musyoka amemtaka Rais
William Ruto kuharakisha mchakato wa uteuzi wa makamishna wapya wa Tume Huru ya
Uchaguzi na Mipaka (IEBC) akisema kutokuwepo kwa makamishna hao kunawanyima
Wakenya haki ya uwakilishi.
Bw Musyoka alisema hayo Jumanne wakati wa Kongamano la
Kitaifa lilokuwa likijadili Kuhusu Kukamilishwa kwa Mageuzi ya mfumo wa
Uchaguzi kuelekea 2027 na kusisitiza kuwa ukosefu wa nia njema ya kisiasa
unazuia utekelezaji wa sheria iliyoundwa Juni 2024 baada ya wabunge kupitisha
Mswada wa marekebisho ya Sheria ya IEBC ya mwaka 2023.
Sheria hiyo inapendekeza kuundwa kwa jopo jipya la
kuteua makamishna wa IEBC lenye wanachama tisa na hivyo kuharamisha uwepo wa
jopo la zamani lenye wanachama saba liloongozwa na Kasisi Daktari Nelson
Makanda.
“Inasikitisha kuwa IEBC bado haina makamishna
watakaotekeleza mageuzi muhimu yanayohusiana na masuala ya uchaguzi, hamna nia
ya kisiasa. Kuingiliwa kwa asasi za umma ndiko kumezuia kuwepo kwa tume halali
itakayoweza kutekeleza majumu yake ya kikatiba,” Alisema Bw. Musyoka.
Bw. Musyoka ameongeza kuwa Majukumu muhimu ya IEBC
ambayo yamekwama ni kama vile kufanyika kwa chaguzi ndogo katika maeneo ya bunge na wadi kadhaa ambazo hazina
wawakilishi pamoja na uwekaji upya wa
mipaka ya maeneo wakilishi na utayarishaji wa sera mbalimbali za kufanikisha
utendaji kazi wa tume hiyo.
Kiongozi huyo wa Wiper pia alilaumu Jopo la Kutatua Mizozo inayohusiana na Vyama vya Kisiasa (PPDT) akisema imekosa kuzingatia kanuni ya usawa wa kijinsia katika uamuzi wake kuhusu uteuzi wa wanachama wa jopo la kuteua makamishna wa IEBC.
Kwa mujibu wa Gazeti la Taifa letu mnamo tarehe 11 septemba 2024 , PPDT
iliamua kuwa jina la Augustus Muli wa chama cha National Labour Party (NLP)
ndio liwasilishwe na Azimio kama mwakilishi wake katika jopo hilo la watu tisa
badala ya Balozi Koki Muli huku Asasi nyingine zinazotarajiwa kuwasilisha
majina ya wawakilishi wao katika jopo hilo ni Chama cha Mawakili Nchini (LSK),
Baraza la Madhehebu Nchini (IRC), Chama cha Mahasibu Nchini (ICPAK) na Tume ya
Huduma za Bunge (PSC).
Hata hivyo Majina hayo yote yanapaswa kuwasilishwa kwa
tume ya PSC kisha yawasilishwe kwa Rais Ruto kwa uteuzi rasmi na baada ya kuteuliwa rasmi wanachama wa jopo
hilo litaapishwa na kuweka matangazo
magazetini kuwaalika Wakenya waliohitimu kuwasilisha maombi ya kutaka kujaza
nafasi ya mwenyekiti wa IEBC na makamishna sita.
IEBC ilisalia bila mwenyekiti na makamishna kuanzia Januari 17, 2023 baada ya aliyekuwa mwenyekiti wake Wafula Chebukati na makamishna Abdi Guliye na Boya Molu kukamilisha muda wao ,badae Desemba 2022 makamishna wengine watatu Juliana Cherera (Naibu Mwenyekiti) pamoja na Francis Wanderi na Justus Nyang’aya walilazimishwa kujiuzulu.
Mwandishi;Harieth Kamugisha
Mhariri;Ellukagha Kyusa
0 Comments