📌Barabara ya Kakonko hadi Mpaka wa Burundi Kujengwa kwa Lami
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Mhe. Dkt. Biteko amesema Serikali inayoongozwa na Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imedhamiria kuipatia Kigoma miradi ya maendeleo na fursa mbalimbali ili kuufungua mkoa huo kiuchumi.
Akihutubia katika mkutano wa hadhara katika Kata ya Kasanda Wilaya ya Kakonko leo Septemba 18, 2024 Dkt. Biteko amesema kuwa Serikali imetekeleza miradi mingi ya maendeleo mfano hospitali na barabara ikilinganishwa na kipindi kilichopita ambapo wananchi walikuwa kitaabika kupata huduma mbalimbali za kijamii.
Awali wananchi wa Kakonko walikuwa wakipata huduma za afya kutoka Hospitali ya Bugando na Geita, uwepo wa hospitali hiyo utasaidia kupunguza gharama ya kufuata mbali huduma za afya.
Pamoja ya hayo, Dkt. Biteko ametoa wito kwa viongozi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) kuendesha mchakato mzuri wa kura za maoni na wachague wagombea wenye sifa na sio kutumia rushwa.
Kwa upande wake, Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Mhe. Zainabu Katimba amesema kuwa Rais Samia amefanya uwekezaji wa zaidi ya shilingi bilioni 4 kwa ajili ya majengo na vifaa tiba katika Hospitali ya Wilaya ya Kakonko, aidha ametoa maelekezo mahsusi kuwa hospitali zote za wilaya nchini ziwe na wodi ya watoto ili kupunguza vifo kwa mama na mtoto.
Imebainishwa kuwa idadi ya Vifo vya watoto wachanga vimepungua kutoka 556 hadi 104 katika vizazi hai 100,000.
Amesema mafanikio hayo ni matokeo ya jitihada kubwa inayofanywa na Rais Samia kwa ajili ya akina mama nchini,” amesema Mhe. Katimba.
Baadhi ya wananchi wa Kakonko waliojitokeza kumlaki na kumsikiliza Naibu Waziri Mkuu na waziri wa Nishati Dkt. Doto Biteko.
Aidha, amewahimiza wananchi wa Kakonko kujiandikisha katika daftari la wapiga kura na baadae kushiriki katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika Novemba 27, 2024
Naye, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Kakonko na Diwani Kata ya Gwarama, Bw. Fidelis Nderego amesema “ Kakonko tukipata barabara ya kiwango cha lami hadi Soko Kuu la ujirani mwema kati ya Kakonko na Burundi uchumi wa wananchi wa Kakonko na Mkoa wa Kigoma utafunguka kiuchumi.”
Aidha, mkazi wa Kakonko, Maita Paschal amesema kuwa uwepo wa Hospitali hiyo ya Wilaya ya Kakonko unawasaidia wananchi kupata huduma karibu kuliko ilivyokuwa awali ambapo walisafiri umbali mrefu kupata huduma.
Hii ni mara ya kwanza kwa Dkt. Doto Biteko kufanya ziara wilayani Kakonko tangu alipoteuliwa kuwa naibu waziri mkuu na Waziri wa Nishati.
Mwandishi: Immaculate Makilika
Mhariri: Prosper Kwigize
0 Comments