CHUO Kikuu Kishiriki cha Elimu Mkwawa (MUCE) kimewakutanisha wadau mbalimbali wa elimu kutoka ndani na nje ya Tanzania katika kongamano linalolenga kujadili dhana ya elimu ya kujitegemea na umuhimu wake katika maendeleo ya jamii.
Kongamano hilo linalofanyika chuoni hapo kwa kushirikiana na Chuo cha VIA cha Denmark, limefunguliwa rasmi leo Septemba 03,2024 Mkoani Iringa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi, na Teknolojia, Dk Willison Mahera.
Dk Mahera amesema kongamano hilo linatoa fursa ya kuhamasisha taasisi nyingine za elimu nchini kuzingatia umuhimu wa kufundisha elimu inayolenga kujitegemea.
“Kupitia kongamano hili, washiriki na wataalamu watachangia katika kuhakikisha kuwa elimu inayotolewa inawaandaa wanafunzi kuwa na uwezo wa kujitegemea, badala ya kutegemea ajira za kuajiriwa.”Alisema Dr Mahera
Dk Mahera Aliongeza kuwa kongamano hilo
linaendana na mabadiliko ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2023, ambayo
inasisitiza utoaji wa elimu bora inayolenga kuzalisha wahitimu wenye uwezo wa
kujiajiri na kuleta mabadiliko katika jamii zao.
“Lengo la elimu ni kuhakikisha
wahitimu wanapata ujuzi utakaowawezesha kujitegemea. Ndiyo maana Rais Samia
aliagiza kufanyika mapitio ya Sera ya Elimu ya mwaka 2014, na sasa tunayo sera
mpya inayolenga kutengeneza wahitimu wenye uwezo wa kujiajiri,” amesema Dk
Mahera.
Wadau wa Elimu wakifuatilia ufunguzi wa Kongamano la Elimu Chuo kikuu Kishiriki Mkwawa (MUCE) lilofunguliwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Sayansi, na Teknolojia, Dk Willison Mahera.
Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa MUCE, Profesa Deusdedit Rwehumbiza, alisema kongamano hili lina manufaa makubwa kwa chuo hicho, hasa katika juhudi zake za kuendelea kuboresha mifumo ya elimu na miundombinu huku Alitaja mradi wa HEET kama mojawapo ya miradi mikubwa inayofanya mageuzi katika chuo hicho, ikiwemo ujenzi wa majengo mapya na hosteli.
Kongamano hilo la siku mbili linawaleta pamoja watafiti, walimu, na wataalamu mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi, kujadili mada muhimu zikiwemo utoaji wa elimu jumuishi, sayansi na teknolojia, masuala ya kijinsia, ujuzi wa kujitegemea, na uvumbuzi.
Mwandishi:Abel Mahenge
Mhariri: Harieth Dominick
0 Comments