Kura za kutokuwa na imani zamuondoa Waziri wa Ufaransa Madarakani

Wabunge wa Ufaransa wamepiga kura ya kutokuwa na imani na serikali, hatua ambayo imelitumbukiza taifa hilo katika mzozo mkubwa wa kisiasa.

 Wabunge wanaoelemea mrengo mkali wa kulia na wa kushoto waliungana kuunga mkono hoja ya kutokuwa na imani na Waziri Mkuu Michel Barnier, kwa wingi wa kura 331.

Hatua hiyo inamlazimu waziri mkuu huyo kukabidhi barua ya kujiuzulu pamoja na serikali yake kwa Rais Emmanuel Macron,huku  serikali hiyo ikiwa imedumu madarakani kwa miezi mitatu  pekee ikiwa ni miongoni, mwa zile zilizokaa madarakani mwa muda mfupi zaidi tangu mwaka 1958.

 Vyama vya mirengo ya kulia na kushoto vimemuondoa  Barnier kwa kutumia  madaraka yake maalum ya kikatiba kutekeleza sehemu ya bajeti bila kupata idhini ya bunge.

 Kabla ya kura kupigwa, Barnier aliwaambia wabunge kwamba nakisi iliyopo isingeweza kuondoka kwa hoja ya kumuondowa yeye madarakani, na kwamba serikali yoyote itakayokuja baada yake itakumbwa na tatizo hilo la kukabiliana na nakisi ya bajeti.

Waziri Mkuu wa Ufaransa aliyeondoshwa kwa kura ya kutokuwa na imani, Michel Barnier.

Rasimu ya bajeti hiyo ilikuwa inataka euro bilioni 60 ili kuziba nakisi hiyo.

 Hii ni mara ya kwanza kwa serikali kuangushwa kwa kura ya kutokuwa na imani bungeni tangu mwaka 1962. Hatua hii, inatajwa  kuchangiwa  na uamuzi wa Macron kuitisha uchaguzi wa mapema mwezi Juni mwaka huu, ambapo matokeo yake yalikuwa ni bunge lililopasuka likiwa na wabunge wengi kutoka upinzani.

Kutokana na kuporomoka kwa serikali hii, sasa Ufaransa inaelekea kuumaliza mwaka huu bila serikali madhubuti wala bajeti ya mwaka 2025, ingawa katiba inaruhusu kuchukuliwa hatua maalum ambazo zitaepusha kufungwa kabisa kwa shughuli za serikali kama ilivyo kwa Marekani.

 Kwa upande mwengine, mpasuko wa kisiasa wa Ufaransa utaudhoofisha zaidi Umoja wa Ulaya, ambao tayari unakabiliana na kuporomoka kwa serikali ya mseto nchini Ujerumani, 

Mhariri:Harieth Dominick.


Post a Comment

0 Comments