Prof. Palamagamba Ang’aka uharibifu wa Viti Benjamini Mkapa

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Prof. Palamagamba Kabudi amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara hiyo kuchukua hatua mara moja kwa kuwaandikia timu ya Simba SC na kuwanakili Shirikisho la Mpira wa Tanzania (TFF) kugharamikia  uharibifu uliotokea katika uwanja wa Benjamin Mkapa wakati mechi ya Kombe la Shirikisho barani Afrika kati Simba SC dhidi ya SC Sfaxien ya Tunisia zilipwe.

Taarifa hiyo imetolewa Leo na  kitengo cha mawasiliano Serikali kupitia wizara ya Habari, Utamaduni,Sanaa na Michezo imeeleza kuwa wizara imesikitishwa na vitendo vya mashabiki kung’oa na kuharibu viti katika Uwanja wa Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam katika mchezo huo ambao ulipigwa jana Desemba 15, 2024.

Aidha Prof.Kabudi amewataka mashabiki wanaoingia katika Uwanja wa Benjamin Mkapa kuacha vitendo vya uharibifu wa uwanja kwa kuwa wanasababisha hasara kwa Serikali na kuharibu ubora wa uwanja.
"Vitendo vilivyofanyika jana katika Uwanja wa Benjamin Mkapa havikubariki na sio vya kimichezo, nakuelekeza Katibu Mkuu kuchukua hatua mara moja. Pamoja na kuwaandikia Simba Sports Club na TFF, wapeni ushirikiano Polisi ili watu wote waliokuwa wanang'oa viti na kuvitupa wakamatwe na wachukuliwe hatua za kisheria, lazima tabia hii ikomeshwe" amesema Prof. Kabudi.

Baadhi ya mashabiki wakifanya uharibifu katika uwanja wa Benjamin Mkapa
Katika hatua nyingine Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam limethibitisha kutokea kwa fujo katika uwanja wa benjamini mara baada ya mchezo huo kutamatika kwa Simba SC kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi CS Sfaxien ya Tunisia.

Kamanda wa Polisi Kanda ya Dar es Salaam,Jumanne  Muliro Jumanne, amesema fujo hizo zilitokana na mashabiki wa CS Sfaxien kutoridhika na maamuzi ya Refa, ambaye aliongeza dakika 7 kufidia dakika zilizopotea, hatua hiyo ilipelekea Simba SC kupata goli la pili la ushindi.

"Wachezaji wa CS Sfaxien na benchi lao walimfuata Muamuzi na kuanza kumshambulia hali iliyochochea mashabiki wao kufanya uharibifu," Amisema Kamanda Muliro.

Hata hivyo Muliro amebainisha kuwa Shabiki mmoja wa CS Sfaxien ameumia katika vurugu hizo na kupatiwa huduma ya kwanza na jumla ya viti 256  ikiwa viti 156 vya bluu na 100 vya orange vimeripotiwa kung’olewa na mashabiki wa timu hiyo.

Jeshi la Polisi limeahidi kushirikiana na mamlaka za soka kuchukua hatua kali dhidi ya vitendo hivyo visivyokubalika.

Taarifa kutoka Wizara ya habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo




Taarifa kutoka jeshi la polisi kanda maalumu ya Dar Es Salaam

Mwandishi; Sharfat Shinji
Mhariri; Ramadhani Zaidy

Post a Comment

0 Comments